24 May 2015

Fahamu maana ya biashara kwa njia ya intaneti (E-Commerce)

Je, umekuwa ukijiuliza nini maana halisi ya kufanya biashara na kupata kipato kupitia intanet? Au pengine ulikuwa ukijiuliza maswali mengi kuwa unaanzaje kuuza au kununua kwenye intaneti? Hapa utajifunza na kufahamu maana halisi ya ecommerce na jinsi inavyofanya kazi. Mwisho wa siku utakuwa muuzaji au mnunuaji kupitia intaneti. Na kwa maana hiyo utakuwa miongoni mwa mamilioni ya watu ambao wamekamata fursa za kibiashara kutumia intaneti.

Maana ya ecommerce ni kitendo cha kuuza au kununua bidhaa na/au huduma kwa njia ya intaneti. Shughuli hii haijaanza leo bali ilianza miaka ya 1960 baada ya kuibuka teknolojia iitwayo Electronic Data Interchange (EDI) ambapo mfumo huo uliwezesha makampuni au watu kuweza kubadilishana hati, hundi au risiti za kibiashara kwa kutumia komputa zilizounganishwa na intaneti. Shughuli hiyo ilishika kasi zaidi kufikia miaka ya 1990 na mwanzo wa 2000. Mfano mwaka 1995, mtandao wa amazon.com ulianzishwa kwa madhumuni ya kuuza vitabu. Mwaka huohuo mtandao wa ebay.com ulianzishwa ukitoa uwezo wa mtu kuuza bidhaa kwa mtu mwingine. Kwa sasa mitandao hiyo imekua sana kulingana na ongezeko la wadau kutoka duniani kote.

 Makundi makuu ya ecommerce 

 B2B (Business to Business)
 Ni mfumo wa biashara unaohusisha wenye viwanda wakiwauzia wafanya biashara wakubwa wanaouza kwa jumla au kiwanda kwa kiwanda wakiuziana au mfanya biashara wa jumla akimuuzia mfanya biashara mwingine auzaye kwa jumla. Mfano wa masoko hayo ya B2B ni kama alibaba.com, made-in-china.com, globalsources.com, tradett.com na mengine mengi.

 C2C (Consumer to Consumer)
 Huu ni mfumo wa kibiashara ya intaneti ambao unahusisha mtu na mtu wakiuziana bidhaa moja au zaidi. Hapa unaweza kuuza au kununua bidhaa ya aina yoyote hata kama ni ndogo na kwa thamani ndogo. Mfano wa masoko haya ni kama aliexpress.com, ebay.com, craiglist.com, etsy.com na mengine mengi.

 B2C (Business to Consumer)
 Kundi hili linahusisha wauzaji wakubwa au viwanda kuwauzia makundi ya wateja aina zote. Hapa pia hutumika mifumo ambayo hakuna mtu katikati wa kuweza kumwuliza (hadi ikibidi) kwani kila kitu unakuta kimewekwa bayana na hiyo mifumo. Mfano amazon.com na masoko mengine.

 C2B (Consumer to Business)
 Hapa unakuta mtu binafsi (consumer) anaweka bidhaa yake kwa njia ya mnada, kisha makampuni yanashindana dau. Baadae huyu muuzaji binafsi anachagua kampuni gani aiuzie hiyo bidhaa. Mfano wake ni kama elance.com na mengine.

Baada ya kuyaona na kuyatambua hayo makundi ya masoko ya kwenye mtandao, sasa hatua inayobaki ni aidha kujisajiri kwenye soko moja au zaidi kama muuzaji au mnunuaji. Kila soko lina namna yake ya kujiunga na pia lina sera tofauti na jingine. Kwa hali hiyo utakapoamua kujiunga utaangalia kanuni na masharti ya soko husika ili uweze kufanya biashara bila shida yoyote. Pia mifano ya masoko niliyoitoa hapo juu haimanishi kuwa hiyo ndio jumla ya masoko yote duniani, hapana, yapo mengi sana. Hata hapa Tanzania kwa mfano kuna masoko kama zoom, kupatana.com ambayo ni C2C marketplaces. Ukishaamua kufanya biashara kwa intaneti utagundua masoko na fursa nyingine nyingi zaidi.

2 comments:

Tafadhali toa mchango au maoni yako hapa